Tuesday, 25 October 2016

RAIS KENYATTA AFUTILIA MBALI ZIARA YA ANGOLA.

Naibu rais William Ruto atamwakilisha rais katika mkutano huo wa Angola.

Ben Kirui
Rais Uhuru Kenyatta amefutilia mbali ziara yake rasmi ya Angola kutokana na shambulizi la kigaidi lililotokea katika eneo la Mandera usiku wa Jumatatu ambapo watu 12 waliuawa.
Kupitia kwa msemaji wa ikulu Manoah Esipisu, rais amefutilia mbali ziara hiyo ili kukabiliana na shambulio hilo na kuomboleza na familia zilizopoteza wapendwa wao.
Aidha Rais amewahimiza wakenya kuungana pamoja na kushirikiana na walinda usalama kwenye vita dhidi ya ugaidi.
Naibu rais William Ruto sasa ndiye atakayemwakilisha rais katika mkutano huo wa Angola.

Wakati huo huo viongozi kutoka kaunti ya Mandera wamelaani shambulio hilo la kigaidi huku wakisema ufisadi ndio chanzo cha kikithiri kwa uovu huo.
Wakiongozwa na Seneta wa kaunti hiyo Billow Kerrow, wabunge hao wamelaumu Serikali kwa kushindwa kuchukulia suala la usalama wa eneo hilo kwa uzito.

Aidha Seneta huyo amesema utovu wa usalama katika kaunti ya Mandera umeathiri shughuli za maendeleo katika eneo hilo kwani watu wasio wenyeji ndio wamekuwa wakilengwa.

No comments: